Lugha Nyingine
China, Tanzania na Zambia zatoa heshima kwa wahanga wa China katika maadhimisho ya miaka 50 ya TAZARA (2)
DAR ES SALAAM - China, Tanzania, na Zambia zimetoa heshima kwa wataalamu wa China waliojitolea maisha yao wakati wa ujenzi wa Reli ya Tanzania-Zambia (TAZARA) jana Jumanne, zikiadhimisha kumbukumbu ya miaka 50 tangu reli hiyo ianze kufanya kazi kibiashara na kusisitiza dhamira zao kwa ufufuaji wake.
Hafla ya kuweka mashada ya maua ilifanyika kwenye makaburi ya wataalamu hao wa China jijini Dar es Salaam, ambapo watu wapatao 100 walivumilia mvua ya asubuhi kuwakumbuka wahandisi, mafundi, na wafanyakazi 70 wa China waliopoteza maisha yao wakati wa ujenzi wa reli hiyo inayounganisha Tanzania na Zambia na kusaidia kuiendeleza Afrika.
Balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian amesema wafanyakazi zaidi ya 50,000 wa China walijiunga na wenzao wa Tanzania na Zambia katika kujenga reli hiyo, ambayo inajulikana sana kwa jina la "Reli ya Uhuru" na "Reli ya Urafiki," wakishinda changamoto kubwa kupitia moyo wa mshikamano na urafiki.
Amesema moyo wa TAZARA, wenye sifa ya kuheshimiana, usawa, kuhimili magumu, na ushirikiano wa kimataifa usio na ubinafsi, unaendelea kutumika kama nguvu endeshi kwa ushirikiano kati ya China na Afrika.
Balozi Mkuu wa Zambia nchini Tanzania Mathews Jere ameielezea TAZARA kuwa ni ishara ya matumaini ambayo iliipa Zambia isiyo na bahari lango muhimu la kuifikia bahari, ikionyesha maono ya pamoja ya viongozi waanzilishi Julius Nyerere na Kenneth Kaunda.
Mkurugenzi Mtendaji wa TAZARA Bruno Ching'andu amesema reli hiyo inabaki kuwa ukumbusho wa kudumu wa kujitolea na ushirikiano, akiongeza kuwa kuhakikisha huduma yake inaendelea kwa watu ni heshima kubwa kwa wale walioijenga.
Lu Haiqiang, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Uhandisi wa Ujenzi la China Tawi la Afrika Mashariki, amezungumzia juhudi zinazoendelea za kuifanya reli hiyo kuwa ya kisasa kufuatia ahadi ya pamoja ya kufufua ushoroba huo na kufungua fursa mpya za kiuchumi katika njia yake, akiongeza kuwa kazi hiyo ya kufufua imedumisha kasi tulivu.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma




