Kukita Mizizi Barani Afrika | Mahojiano Maalum na Liu Hongwu, Mkuu wa Taasisi ya Stadi za Afrika, Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Septemba 08, 2026

BEIJING —Septemba 2, Semina juu ya Stadi za Eneo la Afrika Kuhudumia Mikakati ya Kitaifa na Ujengaji wa Uwezo wa Mawasiliano ya Kimataifa wa Taasisi ya Washauri Bingwa wa China-Afrika ilifanyika Beijing. Miongoni mwa washiriki alikuwa Liu Hongwu, Mkuu wa Taasisi ya Stadi za Afrika katika Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang, ambaye ametumia miongo minne akifanya stadi mbalimbali kuhusu Afrika. Katika mahojiano na People’s Daily Online, Liu ametoa maoni yake kwamba mfumo wa maarifa uliojengwa kwa pamoja na wasomi wa China na Afrika umekuwa moja ya matokeo muhimu zaidi ya ushirikiano wa pande mbili.

Liu Hongwu (katikati) akihutubia semina hiyo. (Picha/Hu Wentao)

Liu Hongwu (katikati) akihutubia semina hiyo. (Picha/Hu Wentao)

Kitabu Kilichoandikwa Kutoka Mitazamo Mitatu

Jambo muhimu la semina hiyo lilikuwa ni uzinduzi wa Kitabu cha Tathmini ya Pande Mbalimbali ya Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika, kilichohaririwa kwa ushirikiano na Liu na wasomi wawili wa Afrika: Isaac Bazié wa Burkina Faso, rais wa zamani wa Jumuiya ya Masomo ya Kiafrika ya Canada, na Fikresus Amazion wa Eritrea, afisa wa muda mrefu katika Umoja wa Afrika.

Kitabu hicho chenye sura 12 kinaleta pamoja wasomi kutoka pande tatu—China, Afrika, na Magharibi—kufanya masomo kuhusu Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC), mfumo ulioanzishwa mwaka 2000. Liu anaona umuhimu wa kitabu hicho katika mambo mawili: kinavuka mipaka ya jadi ya taaluma ili kufafanua masuala ya nyakati za sasa, na kinatoa mitazamo mitatu tofauti kutoka China, Afrika, na Magharibi, hali ambayo inawapa wasomaji picha kamili zaidi kuliko ambayo inaweza kutolewa na upande wowote mmoja.

Katika kipindi cha miaka 25 iliyopita, ajenda ya FOCAC imepanuka kutoka miundombinu na kupunguza umaskini hadi mageuzi ya viwanda, utawala wa kitaifa, na zaidi. Kwa kufungamanisha utafiti wa sera, masomo ya kitaaluma, na uchambuzi wa taasisi ya washauri bingwa, kitabu hiki kinalenga kusaidia wasomaji kote duniani kuelewa vema namna jukwaa hili linavyofanya kazi na kile ambacho limefanikisha.

Kutoka Kufuata Hadi Kuongoza

Nyuma ya kitabu hiki kuna lengo kabambe zaidi: kusaidia wasomaji wa Afrika kuelewa ushirikiano kati ya China na Afrika kupitia sauti za Afrika. Liu amekumbushia kwamba wakati alikuwa akisoma Afrika miaka mingi iliyopita, alitafuta kwenye maktaba za vyuo vikuu na maduka ya vitabu ili kupata vitabu kuhusu China—na hakuweza kupata hata kimoja, isipokuwa vitabu vichache vilivyoandikwa na wasomi wa Magharibi. "Wakati huo, wasomaji wa China na Afrika walijuana kupitia vitabu vilivyoandikwa na wasomi wa Magharibi," amesema.

"Tuna mabadilishano ya moja kwa moja kati yetu, na tunapaswa kuandika kuhusu uhusiano kati ya China na Afrika pamoja." Matumaini yake ni kwamba rafu za vitabu za Afrika siku moja zitabeba vitabu vingi zaidi vilivyoandikwa na wasomi wa China na Afrika wenyewe.

Liu aliweka tumaini hilo katika vitendo mwaka 2011, alipoanzisha Jukwaa la Taasisi za Washauri Bingwa la China-Afrika, ambalo sasa ni mfumo rasmi ungaji mkono wa FOCAC. Kwenye mkutano wake wa 13 mwaka 2024, wasomi kutoka taasisi za washauri bingwa zaidi ya 50 za China na Afrika walitoa kwa pamoja Makubaliano ya Dar es Salaam, mfumokazi kwa ajili ya ushirikiano wa Nchi za Kusini mwa Dunia juu ya maendeleo, usalama, na utawala.

Zaidi ya jukwaa hili kinara, Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang kimesaidia kuanzisha Jukwaa la Abuja nchini Nigeria, Jukwaa la Sudan Kusini, na majukwaa mengine mahsusi ya nchi kupitia kushirikiana na nchi zaidi ya kumi za Afrika, zikiwemo Misri, Tanzania, na Togo -- yote yakiwa yamejengwa kwa ushirikiano na wasomi wa China na Afrika. Kwa Liu, ufanisi wa masomo ya Kiafrika nchini China unategemea kanuni rahisi: ubadilishanaji sawa. Wasomi wa China, anasema, lazima kwanza waielewe Afrika kiuhalisia na kupata kutambuliwa huko kabla ya mfumo wa kuchangia maarifa kuundwa.

Miongo minne, na Jina la Kiafrika

Liu amejitolea kwa miaka arobaini kwenye masomo ya Afrika, na kazi zake za kiutafiti zimempeleka katika nchi zaidi ya 30. Mwaka 1990, alisoma katika Chuo Kikuu cha Lagos nchini Nigeria chini ya mwanahistoria Ebiegberi Joe Alagoa. Miongo kadhaa baadaye, wakati Liu aliporudi kwenye Delta ya Niger kumtembelea mwalimu wake mzee, Alagoa ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka tisini alimpa jina la Ijaw—jina kutoka kabila la wenyeji linalomaanisha “aliyerudi.”

Safari zake katika bara zima hilo zimempa marafiki wengi, kutoka viongozi wakuu wa nchi hadi raia wa kawaida. Miongoni mwa simulizi anazozithamini zaidi ni ile aliyoisikia moja kwa moja kutoka Nelson Mandela.

Mandela alisimulia, wakati wa kifungo chake kwenye Kisiwa cha Robben, katika tarehe 1, Oktoba kila mwaka, Siku ya Taifa ya China, wanachama wa ANC walikuwa hupeana mikono mara tatu kila walipokutana, "kwa sababu tuliiona China kuwa tumaini la Afrika." Uhusiano huu wa mshikamano, unaoanzia kutoka maelfu ya maili, ulimgusa moyo sana Liu.

"Watu wa Afrika ni wa dhati na wenye moyo wa ukarimu, na wamejaa ndoto kama Wachina," amesema. "Ni wasomi hawa wa Afrika ambao wameniwezesha kujitolea maisha yangu kwa Afrika."

Kwa Liu, jambo la furaha zaidi maishani mwake ni marafiki wengi wa Afrika aliowapata katika kipindi hicho cha miaka mingi. Machoni pake, uhusiano kati ya China na Afrika si dhana dhahania ya kidiplomasia bali ni jumla ya ubadilishanaji wa ana kwa ana. Kadri wasomi wengi zaidi wa Afrika wanavyochukua ujivuni katika kushirikiana na wenzao wa China, uelewa wa kina na wenye usawa zaidi wa uhusiano kati ya China na Afrika — ambao unatokana na sauti nyingi badala ya simulizi moja — hatua kwa hatua unaanza kuchukua sura.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha