Trump asema Marekani iko tayari kwa mashambulizi zaidi ya anga dhidi ya Iran, akanusha mipango ya kuupa jina lake Mlango Bahari wa Hormuz

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Septemba 03, 2026

WASHINGTON - Jeshi la Marekani liko tayari kuanzisha mashambulizi zaidi dhidi ya Iran "wakati wowote tunaotaka," Rais wa Marekani Donald Trump amesema.

"Lilikuwa ni shambulio kali sana jana usiku, na tumejitayarisha kufanya jingine wakati wowote tunaotaka," Trump amewaambia waandishi wa habari jana Jumatano katika Ikulu ya White House.

Jeshi la Marekani "limeharibu vifaa vyote vipya ambavyo walijaribu kuweka kando ya Mlango Bahari wa Hormuz," amesema Trump.

Maafisa wa Iran walisema mapema siku hiyo ya Jumatano kwamba shambulio hilo la Marekani la Jumanne usiku lilishambulia sherehe ya harusi kusini mwa Iran, na kuua angalau watu wanne na kujeruhi wengine wengi.

Kamandi ya Kati ya Jeshi la Marekani imesema jana Jumatano kwamba ilikuwa ikichunguza ripoti hizo na kwamba jeshi la Marekani "halilengi raia kamwe."

Alipoulizwa Jumatano alasiri kama kweli alikusudia kuupa Mlango Bahari wa Hormuz jina lake mwenyewe, Trump amesema: "Hapana, hapana ... ilikuwa ni wazo lililotolewa tu."

Trump alitoa wazo la kuipa jina jipya njia hiyo ya maji ya kimkakati mapema Jumatano, chini ya wiki moja baada ya kusaini amri tendaji ya kubadili jina la Ziwa Ontario kuwa "Ziwa Amerika" katikati ya mivutano inayozidi kupamba moto kati ya Marekani na Canada juu ya mizozo ya ushuru wa forodha.

"Sasa kwa kuwa tunao chini ya udhibiti wa Marekani, je, tunapaswa kubadilisha jina la Mlango-Bahari wa Hormuz kuwa Mlango-Bahari wa TRUMP???" Trump aliandika katika ujumbe wake kwenye mtandao wa kijamii wa Truth Social.

Trump aliuambia mkutano huko Long Island mwezi uliopita kwamba atautangaza mlango bahari huo kuwa eneo la Marekani, vyombo vya habari vya Marekani viliripoti.

"Baada ya kuishinda Iran -- ambayo inashindwa vibaya sana -- hivi karibuni nitautangaza Mlango-Bahari wa Hormuz kuwa eneo la Marekani," Trump alisema.

(Wahariri wa tovuti:Liu Mengxue,Renato Lu)

Picha