Lugha Nyingine
IRGC ya Iran yasema imeanza kulipiza kisasi kwa mashambulizi makali ya Marekani

Moshi ukifuka baada ya milipuko kusikika katikati ya jiji la Tehran, Iran, Aprili 1, 2026. (Xinhua/Shadati)
TEHRAN/AMMAN – Vikosi vya Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (IRGC) vimesema jana Jumanne usiku vilianza mashambulizi dhidi ya kambi na mali za Marekani katika eneo hilo kwa kulipiza kisasi kwa mashambulizi ya Marekani dhidi ya majimbo ya kusini mwa Iran mapema siku hiyo, ambayo yamesababisha vifo vya watu watano na kujeruhi wengine zaidi ya 50.
Katika taarifa iliyochapishwa kwenye chombo chake rasmi cha habari cha Sepah, IRGC imesema "jibu litakalowafanya wavamizi kujutia" limeanza, ikisema kuwa mfumo wake wa ulinzi wa anga umedungua droni ya MQ-9 Reaper ya Marekani iliyokuwa na nia ya uhasama.
IRGC imesema vikosi vyake vya anga pia vimerusha makombora ya balistiki na droni kwenye Kambi ya Titin nchini Jordan na kambi ya jeshi la anga ya Shaikh Isa nchini Bahrain, ambayo yameripotiwa kuua "idadi kubwa" ya wanajeshi wa Marekani na kuharibu vifaa kadhaa muhimu na helikopta za kivita.
Imesisitiza kuwa mashambulizi hayo ya Marekani yatarefusha tu muda wa kufungwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz na kuvifanya vikosi vya jeshi la Iran kuazimia zaidi "kukandamiza vikosi vya kigeni vinavyoingilia njia hiyo ya maji."
IRGC imesema mashambulizi hayo yameanza baada ya Marekani kushambulia kwa mabomu maeneo kadhaa ya kiraia kwenye mwambao wa kusini mwa Iran "kutokana na kukata tamaa" na katika kulipiza kisasi kwa shambulio la "kihalifu" na baya la Marekani kwenye sherehe ya harusi katika Jimbo la Hormozgan.
Vikosi vya Jeshi la Jordan – Jeshi la Kiarabu (JAF) vilisema baadaye kuwa mifumo ya ulinzi wa anga ya nchi hiyo Jumanne jioni ilizuia na kuharibu makombora 10 kati ya 13 ya balistiki yaliyoingia anga ya nchi hiyo kutoka Iran katika kipindi cha saa zilizopita.
Kwa mujibu wa JAF makombora mengine matatu yalianguka katika maeneo ya pembezoni mbali kutoka kwenye vituo vya wakazi, huku kukiwa hakuna majeruhi au upotevu wa maisha ulioripotiwa.
Shirika la habari la Fars ya Iran limemrejelea Ahmad Nafisi, naibu mkuu wa Hormozgan anayeshughulika na masuala ya kisiasa na usalama, akisema kuwa watu wasiopungua watano, akiwemo mtoto wa miaka minne na mwanamke mmoja, wameuawa na wengine zaidi ya 50 wamejeruhiwa kwenye shambulio hilo la Marekani lililolenga sherehe ya harusi katika kaunti ya Sirik.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



