Trump asema makubaliano yamefikiwa juu ya kupokonywa silaha kabisa kwa Hamas na makundi mengine yenye silaha huko Gaza

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Julai 31, 2026

WASHINGTON - Rais wa Marekani Donald Trump amedai kwenye mtandao wa kijamii kwamba kile kinachoitwa Bodi ya Amani kimefikia makubaliano ya "kupokonywa silaha kabisa" kwa Hamas na makundi mengine yote yenye silaha huko Gaza jana Alhamisi.

"Makubaliano haya ni hatua muhimu kuelekea Gaza hatimaye kutawaliwa na serikali mpya ya Palestina ambayo itafanya kazi kwa karibu na Bodi ya Amani kusaidia watu wa Palestina," Trump ameandika kwenye mtandao wa kijamii wa Truth Social.

"Wakati huo huo, Israel itakuwa na usalama inaostahili, huku Gaza ikiwa haitumiki tena kuwa kituo cha mashambulizi ya kigaidi," ameongeza.

Makubaliano hayo yatatekelezwa kwa awamu zilizopangwa, kwa mujibu wa Trump, ambaye amebainisha kuwa pale kupokonywa silaha kutakapokamilika, vikosi vya Israel vitajiondoa, na Kikosi cha Kimataifa cha Kuleta Utulivu kitashirikiana na kikosi kipya cha polisi wa Palestina kuchukua jukumu la usalama wa Gaza.

Amesema Misri, Qatar na Uturuki zimesaidia kufanikisha makubaliano hayo kama wapatanishi.

Katika habari iliyotangazwa na televisheni ya serikali ya Misri mapema leo Ijumaa Hamas na makundi ya Palestina yamekubaliana juu ya mpango wa kutekeleza awamu ya pili ya makubaliano ya kusimamisha mapigano Gaza, ikiwemo mchakato wa hatua kwa hatua wa kuorodhesha na kuhifadhi silaha zao.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha