Tanzania yatoa tahadhari juu ya mafuriko katika msimu wa mvua wa Machi hadi Mei

(CRI Online) Februari 06, 2026

Mamlaka ya Hali ya Hewa ya Tanzania (TMA), Alhamisi ilitoa utabiri wake wa hali ya hewa kwa msimu wa mvua unaoanzia Machi hadi Mei 2026, ikitahadharisha juu ya mafuriko yanayoweza kutokea.

Kwa mujibu wa taarifa ya TMA, mvua zitakazonyesha kwa viwango vya kawaida hadi vya juu ya kawaida zinatarajiwa katika pwani ya kaskazini na Bonde la Magharibi la Ziwa Victoria. Hata hivyo, TMA imeeleza kuwa nyanda za juu za kaskazini mashariki na sehemu za Bonde la Ziwa Victoria zinatarajiwa kupata mvua ya viwango vya kawaida hadi chini ya kawaida.

Taarifa hiyo imesema mvua hizo zinatarajiwa kuanza kati ya mwisho wa Februari na katikati ya Machi, huku Aprili ikitarajiwa kushuhudia mvua kubwa zaidi.

Mamlaka hiyo imetahadharisha kwamba maeneo yatakayopata mvua kubwa yanaweza kukabiliwa na mafuriko na uharibifu wa miundombinu, huku maeneo makavu yanaweza kupata upungufu wa viwango vya maji, na kuathiri umwagiliaji na uzalishaji wa umeme kwa nishati ya maji.

Imeongeza kuwa hatari za kiafya pia zinatarajiwa, zikiwemo za milipuko ya magonjwa yanayoenezwa na wadudu na maji kutokana na uchafuzi wa maji wakati wa mvua kubwa na utegemezi unaoongezeka wa vyanzo vya maji visivyo salama katika maeneo makavu.

(Wahariri wa tovuti:Zhao Jian)

Picha