Tanzania yaahidi kuimarisha uhuru wa mahakama na kutumia AI mahakamani

(CRI Online) Februari 03, 2026

Serikali ya Tanzania imesisitiza tena dhamira yake ya kuimarisha uhuru wa mahakama ikiwa ni sehemu ya msingi wa ujenzi wa taifa.

Ahadi hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Tanzania Emmanuel Nchimbi wakati akimwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan kwenye hafla ya kitaifa ya Siku ya Sheria iliyofanyika siku ya Jumapili mjini Dodoma, ambapo amesema uhuru wa mahakama ni muhimu kwa mahakama kutekeleza majukumu yake ya kikatiba na kuhimiza ustawi wa taifa.

Nchimbi amebainisha kuwa serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya mahakama, kuimarisha rasilimali watu, na kuboresha ustawi wa wafanyakazi ili kuleta huduma za haki karibu na watu.

Kwa upande wake Jaji Mkuu wa Tanzania George Masaju amesema mahakama inapanua matumizi yake ya teknolojia ili kuongeza ufanisi, akibainisha kuwa mfumo unaotegemea AI unatengenezwa ili kurekodi, kunakili, na kutafsiri kesi za mahakama kwa wakati halisi.

Amesisitiza kuwa mfumo huo utapunguza kwa kiasi kikubwa ucheleweshaji na dosari katika utunzaji wa kumbukumbu zinazoandikwa kwa mikono, ikiashiria hatua moja mbele katika kuboresha mfumo wa kisheria wa Tanzania.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha